Thesis and dissertation

Browse

Recent Submissions

Now showing 1 - 5 of 53
  • Item
    KAULI ZA NASAHA KATIKA HARUSI ZINAVYOJENGA UHUSIANO WA WANANDOA:
    (SUZA, 2021-12-01) BIROLI,FATMA YAKOUT
    Utafiti huu ulikuwa na lengo la kuchunguza kauli za nasaha katika harusi za Wapemba jinsi zinavyojenga uhusiano wa wanandoa. Utafiti ulikuwa na malengo mawili: Kuainisha kauli za nasaha anazopewa biharusi na bwanaharusi kwa mujibu wa utamaduni wa jamii ya Wapemba na kufafanua uhusiano wa ndoa unaojengwa na kauli hizo. Utafiti uliongozwa na nadharia ya uchambuzi makini wa matini. Utafiti ulifanyika katika wilaya mbili, Chake chake na Mkoani. Data zilikusanywa kupitia mbinu ya dodoso, usaili na ushuhudiaji. Sampuli ya watafitiwa thelathini (30) ilitumika. Utafiti umebaini kuwa kauli za nasaha zitolewazo katika harusi za Wapemba. Ziko kauli za nasaha ambazo zimefanana na zinajenga uhusiano baina ya biharusi na bwanaharusi katika maisha ya ndoa. Mfano “Jihadhari sana, usimruhusu mke kuwa na marafiki wengi na kutumia muda mwingi nje kwa kukaa na marafiki zake.” “Tahadhari sana na ulimi, tunakunasihi, ulimi wako unatakiwa utumie vizuri.” Pia mtafiti amegundua kauli za nasaha zimefanikiwa kuonesha uhusiano unaojengwa na kauli hizo kwa bwanaharusi na biharusi. Mfano wa kauli za nasaha zinazojenga uhusiano kwa bwanaharusi na biharusi: “Tunakunasihi, mke ni mkeo, ndio mwenzio usimfanyie jeuri wala dharau.” “Zingatia vizuri tunayokunasihi, umuheshimu mumeo umuone ni mumeo wala simdharau.” Mtafiti anapendekeza kuwa kauli za nasaha ziendelee kutumika katika jamii ya Wapemba na jamii nyengine za Waswahili. Pia mtafiti anapendekeza uchunguzi zaidi ufanyike katika uwanja wa kitaaluma utakaohusisha kauli za nasaha katika miktadha tafauti ikiwemo msibani, maofisini, mashuleni na miktadha mengineo ili kuzijenga jamii kuwa na maadili bora katika sehemu zote napokuwepo. Pia mtafiti anapendekeza watafiti wengine waangalie kauli za nasaha walizopewa wanandoa wakongwe na wanandoa wa sasa halafu walinganishe wepi waliofanikiwa kudumu katika ndoa zao.
  • Item
    TATHMINI YA UTOAJI WA MAELEZO YA UTAMADUNI KATIKA KUFUNDISHA KISWAHILI KAMA LUGHA YA KIGENI
    (SUZA, 2019-12-01) ALI,Yakuti Nassor
    Utafiti huu umeshughulikia; Tathmini ya Utoaji wa Maelezo ya Utamaduni katika Kufundisha Kiswahili kama Lugha ya Kigeni. Maelezo ya utamaduni ni kipengele muhimu sana katika ufundishaji wa lugha. Maelezo hayo yamebainishwa kwa ufupi katika vitabu kulingana na mada husika. Mwalimu amepewa nafasi ya kutoa maelezo ya ziada kuhusu utamaduni kwa kutumia mbinu alimbali. Utafiti umefanywa Unguja, Mkoa wa Mjini Magharibi katika Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar (SUZA) na Taasisi ya Kiswahili na Utamaduni (KIU). Lengo la utafiti huu lilikuwa ni kubainisha aelezo ya utamaduni yanayotolewa katika ufundishaji wa Kiswahili kama lugha ya kigeni, kutathmini mbinu anazotumia mwalimu kutoa maelezo ya utamaduni katika kufundisha Kiswahili kama lugha ya kigeni na kueleza umuhimu wa maelezo ya utamaduni katika kufundisha Kiswahili kama lugha ya kigeni. Jumla ya watoa taarifa tisa (9) walihusiswa kutoa taarifa katika utafiti huu. Watoa taarifa hao ni walimu wanaofundisha Kiswahili kama lugha ya kigeni ambao walichaguliwa kwa kutumia sampuli lengwa kulingana na upatikanaji wao. Data zilikusanywa kwa kutumia mbinu ya mahojiano, ushuhudiaji na uchambuzi ws nyaraka. Utafiti uliongozwa na nadharia ya utamaduni jamii iliyotumika kuangalia maelezo ya utamaduni kama kitu kipya na muhimu nachotakiwa kupewa mwanafunzi katika ufundishaji lugha na mbinu za utoaji wa maelezo ya utamaduni katika kufundisha Kiswahili kama lugha ya kigeni. Utafiti ulitathmini na kushughulikia utoaji wa maelezo ya utamaduni kwa wanafunzi wa kiwango cha kwanza. Matokeo ya utafiti yamebaini kuwa: walimu wanatumia mbinu mbalimbali kutoa maelezo ya utamaduni lakini mbinu zinazotumika haziwasaidii sana walimu kufundisha wanafunzi wa kiwango cha kwanza kwa urahisi zaidi. Utafiti umependekeza walimu wapewe mafunzo ya kutosha kuhusu utoaji wa maelezo ya utamaduni na matumizi ya mbinu ya teknolojia katika utoaji wa maelezo ya utamaduni kama vile televisheni na mkazo zaidi utolewe kwa walimu wanaofundisha wanafunzi wa kiwango cha kwanza
  • Item
    TATHMINI YA MAZINGIRA YA KIJAMII KATIKA KUJIFUNZA KUSOMA KISWAHILI KWA WATOTO WA KIGENI ZANZIBAR
    (SUZA, 2019-12-01) ALI,Msellem Mohammed
    Utafiti huu umetathmini Mazingira ya Kijamii katika kujifunza kusoma kwa watoto wa kigeni wanaojifunza Kiswahili kama lugha ya kigeni Zanzibar. Jumla ya watoa taarifa 28 walishiriki katika utafiti huu waliogawanyika katika makundi mawili: wajifunzaji lugha 16 na wazazi/walezi wao 12. Utafiti ulifanyika katika skuli ya Kimataifa ya Feza iliyopo Mjini Magharib Zanzibar na katika kaya za wazazi/walezi wa wajifunzaji lugha ya Kiswahili zilizopo Mjini Magharib. Katika kukusanya data, utafiti umetumia kipimo cha kusoma ili kubaini uwezo walionao watoto wa kigeni katika kusoma matini za Kiswahili pamoja na mbinu ya usaili kubaini dhima ya Mazingira ya Kijamii. Aidha, utafiti ulitumia hojaji za kuchunguza mambo ya Mazingira ya Kijamii wa watoto wa kigeni. Utafiti huu uliongozwa na Nadharia ya Ukuzaji Stadi ya Kusoma ya Clay (1966) na Holdaway (1979). Hoja kuu ya nadharia hii ni mchangamano wa kimazungumzo na kusoma pamoja baina ya anayejifunza kusoma na wajuzi wa lugha husika. Vilevile, mchangamano baina ya mjifunzaji kusoma na vitabu vya lugha lengwa ni miongoni mwa misingi mikuu ya ujifunzaji kusoma kwa mujibu wa Nadharia ya Ukuzaji Stadi ya Kusoma. Matokeo ya utafiti yanaonesha kwamba dhima ya Mazingira ya Kijamii katika kujifunza kusoma Kiswahili kwa watoto wa kigeni ni kuwawezesha watoto kupata kuchanganyika na marafiki wanaojua Kiswahili wakiwa katika Mazingira ya Kijamii. Aidha, kuchanganyika na wazazi/walezi wanaotumia Kiswahili pamoja na tabia binafsi ya watoto kujisomea maandiko ya Kiswahili wakiwa katika Mazingira ya Kijamii pia vimechangia uwezo wa kusoma walionao watoto wa kigeni. Vilevile, imependekezwa kwa watafiti wengine kufanyika utafiti kuhusu ufundishaji na ujifunzaji wa stadi nyengine za lugha ya Kiswahili katika Mazingira ya nje na ndani ya darasa.
  • Item
    MKABALA UNAOTUMIKA KATIKA UTUNGAJI WA MITIHANI YA KISWAHILI KAMA LUGHA YA KIGENI:
    (SUZA, 2020-12-01) MGASHO,Makame Sheha
    Utafiti huu unahusu Mkabala Unaotumika Katika Utungaji wa Mitihani ya Kiswahili Kama Lugha ya Kigeni: Mfano Chuo Kikuu Cha Taifa Cha Zanzibar. Utafiti huu uliongozwa na malengo mahsusi matatu. Kwanza kufafanuakwa kiasi gani walimu wanaotunga maswali ya mitihani ya Kiswahili kwa wageni wanavyoifahamu mikabala ya utungaji mitihani. Pilikubainisha aina ya mkabala unaotumika zaidi katika utungaji wa maswali ya mitihani ya Kiswahili kw wageni. Tatu kuchunguza mtazamo wa walimu juu ya mkabala wanaoutumia zaidi katika utungaji wa maswali ya mitihani ya Kiswahili kwa wageni. Utafiti huu ulifanywa katika Idara ya Kiswahili kwa Wageni Chuo Kikuu Cha Taifa Cha Zanzibar. Nadharia iliyotumika katika utafiti huu ilikuwa Nadhari ya Tabia ya Umoja (Unitary Trait Hypothesis) kama ilivyoasisiwa na Oller (1979).Misingi mikuu ya nadharia hii ni kuipima lugha kwa njia ya mjumuishi pamoja na uzingatiaji wa mazingira halisi ya watumiaji wa lugha inayohusika wakati wa upimwaji wake.Sampuli ya utafiti huu ilikuwa ni walimu saba wanaosomesha Kiswahili kwa wageni, watoa taarifa hao walipatikana kwa usampulishaji tajwa. Mbinu zilizotumika ni mbinu ya dodoso kwa ajili ya kukusanya data za lengo la kwanza hadilengo la tatu, na mbinu ya uchambuzi wa nyaraka ilitumika kwa ajili ya kukusanya data za lengo la pili tu la utafiti huu. Matokeo ya utafiti huu yalieleza kwamba walimu wanaosomesha Kiswahili kwa wageni wanaufahamuwa mikabala ya utungaji mitihani ya Kiswahili kama lugha ya kigeni kwa asilimia 57%. Pia utafiti ulionesha kwamba mkabala unaopima stadi nyingi za lugha kwa wakati mmoja ndio ambao hutumika zaidi, na mtazamo wa walimu kuhusu mkabala unaotumika zaidikwamujibu wa matokeo ya utafiti ni wenye kufaa kwani unawapatia matokeo wanayoyahitaji katika upimaji wa Kiswahili kama lugha ya kigeni. Utafiti huu ulitoa mapendekezo ya kwamba walimu waongeze taaluma yao juu ya mikabala ya upimaji, pamoja na uzingatiaji wa stadi zotekuunne za lugha katika upimaji wa wanafunzi ili kuhakikisha kwamba hakuna stadi ya lugha hata moja ambayoinaachwa nyuma wakati wa upimaji wa wanafunzi.
  • Item
    UCHESHI KATIKA UFUNDISHAJI WA KISWAHILI KWA WAGENI:
    (SUZA, 2021-12-01) MOHAMED,Khadija Tahir
    Utafiti huu unahusu Ucheshi katika Ufundishaji wa Kiswahili kwa Wageni ambao umeangazia zaidi katika matumizi ya katuni katika stadi ya mazungumzo. Lengo kuu la utafiti huu ni kuchunguza matumizi ya katuni kama sehemu ya ucheshi wakati wa ufundishaji wa Kiswahili kwa wageni. Malengo mahasusi yalikuwa ni kubainisha aina za katuni zinazotumika katika kufundishia Kiswahili kwa wageni, kuchambua athari zinazotokana na matumizi ya ushechi wa katuni wakati wa kufundisha, kuchambua mbinu zinazotumika kuwasilisha maudhui kupitia katuni darasani na kutathmini mitazamo ya wanafunzi kwenye matumizi ya ucheshi wa katuni katika ufundishaji.Utafiti uliongozwa na nadharia za Ucheshi (Theory of Humours) pamoja na nadharia yamodeli ya ufuatilizi (Monitor Model). Utafiti umetumia mkabala wa kimaelezo naumefanywa ndani ya wilaya ya Mjini katika mkoa wa Mjini Magharibi visiwani Zanzibar. Walengwa wa jumla walikuwa ni walimu wenye uzoefu kuanzia miaka mitatu na kuendelea ambao walichaguliwa kwa mtindo wa usampulishaji nasibu. Sampuli ilikuwa ni walimu watano (5) waliokuwa na wanafunzi kipindi ambacho data zinakusanywa. Aidha utafiti umetumia mbinu ya uchunguzi, usaili na uchambuzi wa nyaraka ili kupata data zenye kuaminika. Uchunguzi ulifanyika ndani ya Idara ya Kiswahili kwa Wageni ya Chuo Kikuu cha Zanzibar. Matokeo ya utafiti yamebaini kuwepo kwa aina mbili za katuni zinazotumika katika ufundishaji wa Kiswahili katika chuo cha SUZA (katuni mjongeo na katuni tuli). Aidha ucheshi katika katuni umeonesha athari kubwa kwa wanaojifunza Kiswahili kama lugha ya kigeni na athari hizo zimegawanywa katika aina mbili athari chanya na athari hasi, kwa upande wa thari chanya ni kujenga misamiati na kupata mitindo ya lugha, kutambulisha utamaduni wa lugha na kuongeza kujiamini kwa wanafunzi, kwa upande wa athari hasi ni muda kuwa mchache na uteuzi wa katuni kuwa mgumu. Mitazamo ya wanafunzi inaashiria kwamba utumiaji wa ucheshi wa katuni katika kufundishia stadi ya mazungumzo huwafanya kufurahia somo na kuvutika nalo na zaidi ya hayo ni kuwapatia kumbukumbu ya muda mrefu ya jambo lililofundishwa darasani. Kulingana na matokeo yaliyopatikana, mtafitialipendekeza kwa Idara ya Kiswahili kwa wageni (SUZA) kushirikiana na wadau mbalimbali wa taaluma na wadau wa maendeleo, kuandaa katuni mahususi kwa ajili ya kufundishia stadi mbali mbali za lugha na sarufi kwa ujumla kupitia usaidizi wa teknolojia. Mapendekezo hayo ni kufuatia kuibuka kwa teknolojia nyingi ambazo zinaweza kutumiwa ili kuendana na ufundishaji wa lugha kimataifa