MITAZAMO YA WALIMU WANAOFUNDISHA KISWAHILI KWA WAGENI JUU YA UTOAJI WA MOTISHA YA NJE

No Thumbnail Available
Date
2022-12-01
Journal Title
Journal ISSN
Volume Title
Publisher
SUZA
Abstract
Utafiti huu ulidhamiria kuchunguza mitazamo ya walimu wanaofundisha Kiswahili kwa wageni juu ya utoaji motisha ya nje. Malengo mahsusi ya utafiti huu ni kubainisha aina za motisha ya nje zinazotolewa juu ya ufundishaji Kiswahili kwa wageni, kufafanua mbinu za motisha ya nje zinazotumika juu ya ufundishaji Kiswahili kwa wageni na kuchambua mitazamo ya walimu juu ya utoaji motisha ya nje wakati wa ufundishaji Kiswahili kwa wageni. Utafiti huu uliongozwa na nadharia ya motisha ya Gardner (1975) na data zilichambuliwa kwa kutumia mkabala wa kimaelezo. Utafiti uliangazia hasa motisha ya nje. Sampuli lengwa ilitumika kuchagua watoa taarifa kulingana na uzoefu na utayari wao. Data zilikusanywa uwandani kwa kutumia shajara na ushuhudiaji. Jumla ya walimu sita (6) wanaofundisha Kiswahili kwa wageni katika Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar walishiriki katika utafiti huu. Matokeo ya utafiti huu yalionesha kwamba kuna motisha zinazotumia maneno na motisha zinazotumia vitendo. Aidha utafiti uligundua walimu wanatumia mbinu mbalimbali wakati wa utoaji motisha ya nje ambazo ni, mbinu ya kuwasifu wanafunzi, kutumia imoji, kutoa zawadi na kuwapongeza wanafunzi. Hatimaye, utafiti ulibaini mitazamo chanya na hasi katika kutoa motisha ya nje. Mitazamo chanya ni kuamsha ari na hamu ya kujifunza zaidi, kuondoa hofu na woga wakati wa kujifunza, kuwa karibu na mwalimu na kuwachangamsha wanafunzi. Kwa upande wa mitazamo hasi ni kuwavunja moyo baadhi ya wanafunzi na kudumaza vipaji vya wanafunzi. Mtafiti aligundua kuwa utoaji wa motisha ya nje ni muhimu katika ufundishaji wa Kiswahili kwa wageni. Hivyo, walimu wanashauriwa kutoa motisha za nje mbalimbali na kutumia mbinu anuai za utoaji motisha ya nje ili kuleta ufanisi katika ufundishaji wa Kiswahili kwa wageni. Utafiti huu umependekeza walimu wapatiwe mafunzo ambayo yatawashajiisha zaidi na utoaji motisha ya nje juu ya ufundishaji wa Kiswahili kwa wageni. Pia uongozi uwashajihishe walimu kutumia mbinu mbalimbali za utoaji motisha ya nje wakati wa ufundishaji wa Kiswahili kwa wageni ambazo zitaweza kuleta tija kwa wanafunzi na kuwaongezea umahiri katika kujifunza.
Description
Mtafiti aligundua kuwa utoaji wa motisha ya nje ni muhimu katika ufundishaji wa Kiswahili kwa wageni. Hivyo, walimu wanashauriwa kutoa motisha za nje mbalimbali na kutumia mbinu anuai za utoaji motisha ya nje ili kuleta ufanisi katika ufundishaji wa Kiswahili kwa wageni. Utafiti huu umependekeza walimu wapatiwe mafunzo ambayo yatawashajiisha zaidi na utoaji motisha ya nje juu ya ufundishaji wa Kiswahili kwa wageni.
Keywords
Citation